Wednesday, August 24, 2011

POLISI WA NIGERIA WAMUOKOA BABA MZAZI WA MIKEL JOHN OBI

Mikel John Obi - kiungo wa Chelsea.
Baba wa mcheza soka kutoka timu ya Chelsea ambaye ni raia wa Nigeria John Mikel aliyetekwa ameachiwa huru na polisi.
Maafisa walivamia kwenye eneo la jirani mjini Kano nchini humo ambapo walimkuta Michael Obi na kuwakamata washukiwa watano.
Michael Obi
Obi alitekwa Agosti 12 alipokuwa akitokea kazini mjini Jos, takriban maili 200 kutoka Kano.
Aliwaambia waandishi wa habari: "Nilianza kuwaomba lakini waliendelea kunipiga bila huruma. Waliniweka sehemu mbaya sana."
Mwandishi wa BBC Yusuf Ibrahim Yakasai alisema uso wake ulionyesha alama za kupigwa ambapo alisema zilitokana na masaibu yaliyomkuta.
Obi alisema, "Nilipelekwa mbali vichakani, katika eneo lililotengwa mjini Jos."
"Wako watano na walikuwa wamevaa mavazi ya kijeshi. Walinisukuma kwenye gari lililopakwa rangi za kijeshi na kuanza kuendesha gari haraka iwezekanavyo. Sikuwahi kujua gari linaweza kupaa namna vile."
Kampuni inayosimamia shughuli za Mikel Sport Entertainment & Media Group (SEM) alisema kwenye taarifa yake: "Mapema leo Michael Obi aliwapigia simu familia yake kuwaeleza kuwa aliachiwa huru na waliomteka."
"John Obi Mikel angependa kuwashukuru wote nchini Nigeria, familia yake na marafiki, Chelsea FC na mashabiki wake kwa yote waliomfanyia wakati wote wa madhila haya."
Wakati baba yake alipokuwa ametoweka, Mikel aliendelea kuichezea Chelsea- akianza na mechi dhidi ya Stoke City na West Bromwich Albion.
Siku ya Ijumaa, meneja wa Chelsea Andre Villas-Boas alimsifu "kwa nguvu za kisaikolojia" zilizoonyeshwa na kiungo huyo kufuatia kutekwa nyara kwa baba yake.

No comments:

Post a Comment